PAROKIA YA MTAKATIFU TERESIA

JIMBO KATOLIKI LA TANGA

Mtakatifu Teresia wa Mtoto Yesu mlinzi wa parokia yetu, utuombee!

 

(Angalia ukurasa huu kwa Kiingereza)

HISTORIA YA PAROKIA

Parokia ya Mtakatifu Teresia ipo ndani ya jiji la Tanga katika vitongoji vya Barabara Ishirini. Hii ni moja ya parokia tatu zilizo katika jiji la Tanga. Parokia hii ilianzishwa mwaka 1953 na ni parokia ya pili kujengwa ndani ya jiji la Tanga ikiifuatia parokia ya Mtakatifu Antoni iliyoanzishwa mwaka.1893. Hapo awali Parokia ya Mtakatifu Antoni iliweza kukidhi mahitaji ya waamini wa mji wa Tanga kwani mji ulikuwa unakuwa polepole na kuwa na asilimia kubwa ya wa-Isilamu.

Baada ya Vita Kuu ya II kulikuwa na ongezeko kubwa la wakazi katika mji wa Tanga na mji ulipanuka sana tokea maeneo ya Chumbageni kuelekeza maeneo ya kusini mwa mji kuelekea Pangani. Kukua huku kwa mji na wakazi wake, kuliongeza hitajiko la kuwa na parokia saidizi kwa wakazi wa maeneo ya kusini mwa mji. Basi eneo la kujenga kanisa lilipatika kati ya nyumba za wananchi katika kitongoji cha Barabara ya Ishirini.

Harakati za ujenzi wa parokia hii zilianza kwa ujengaji wa nyumba ya mapadre katika kitongoji cha Mabawa pembezoni mwa barabara ya kuelekea Pangani. Mheshimiwa padre Bernard MacNally, I.C. alihamishia makao yake katika nyumba hii katika mwaka 1953 kutoka katika nyumba ya mapadre ya Mtakatifu Antoni. Kabla ya kuwa na jengo la kanisa, padre Bernard aliadhimisha ibada ya misa kwenye uwanja wazi karibu na kituo cha polisi cha Mabawa. Baadaye padre Bernard alijenga jengo la kanisa kati ya nyumba za watu katika kitongoji cha Mabawa. Japo eneo hili halikuwa na utulivu mzuri wa kuendesha ibada, lilikuwa ni bora kwa mapadre wamisionari kujizingirisha na maisha ya wenyeji na hivi kujifunza lunga ya ki-Swahili na mila za watu kwa karibu. Ujenzi wa jengo la kanisa la parokia uliendelea hadi kukamilika kwake katika mwaka 1965. Baadaye padre Bernard alijenga nyumba ya mapadre ambayo ilipokamilika ilibadilishwa ikawa nyumba ya masista.

Kutokea parokia ya Mtakatifu Teresia (ambayo imo kusini mwa mji wa Tanga), padre Bernard na mapadre wa parokini hapo walihudumia vigango vyote vilivyokuwa upande huo wa kusini mwa mji. Vigango hivyo vilitawanyika katika mashamba mengi ya mkonge huko Sakura, Kilimangwido, Pangani, hadi kuvuka mto Pangani kwenye vitongoji vya Mkalamo. Iliwachukua muda wa siku mbili kwa mapadre kuweza kusafiri toka Tanga hadi Mkalamo. Kati ya mji wa Tanga na kigango cha Mkalamo kulikuwa na vigango 12 ambavyo viliwalazimu mapadre kuvipatia huduma za kichungaji.

Mheshimiwa padre Bernard MacNally alipewa pia wadhifa wa kuwa makamu wa baba askofu. Alifanya kazi hiyo katika kipindi kigumu cha jimbo wakati afya ya Mhashamu Baba Askofu Arthur ilipokuwa ikiyumba sana na hatimaye kumsukuma kujiuzulu.

Mapadre wazawa wa parokia hii ni: John Mahundi (1985) na Augustine Temu (2007).